Saturday, April 10, 2010

TAMKO LA NCCR MAGEUZI KUHUSU CCM KUPORA KAULI MBIU YA NCCR MAGEUZI. APRILI 10, 2010.

TAMKO LA NCCR MAGEUZI KUHUSU CCM KUPORA KAULI MBIU YA NCCR MAGEUZI.
APRILI 10, 2010.

Watanzania wanafahamu kuwa huu ni mwaka wa uchaguzi mkuu wa Madiwani, Wabunge na Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania. Ni katika msingi huo kila chama cha siasa makini kinapaswa kuandaa Sera, Ilani na Kauli mbiu yake kwa mujibu wa misingi ya Itikadi kama njia ya kuonesha mwelekeo tunapokwenda kwenye uchaguzi.

Ni katika misingi hiyo, Chama Cha NCCR –Mageuzi, kupitia kikao chake cha cha Halmashauri kuu ya Taifa ya Chama kilichoketi Dar es Salaam, Ukumbi wa Msimbazi Centre, Disemba 5-6,2009 pamoja na mambo mengine, kwa misingi ya itikadi yetu ya Demokrasia ya kijamii (Social democrat), tulijadili na kupitisha kauli mbiu(slogan) ya uchaguzi mkuu 2010 kuwa ni “PAMOJA, TUTASHINDA!”.

Hii ni kauli mbiu iliyopitishwa kwenye kikao hicho kwa kuzingatia misingi ya Itikadi yetu ya Demokrasia ya kijamii ambayo msingi wake wa tano ni mshikamano wa kidugu kama iliyoanishwa kwenye katiba yetu. Tunapenda kuutarifu umma kuwa hata baada ya kupitisha kauli mbiu hiyo, chama kiliagiza vifaa vyote kwa ajili ya kampeni za 2010 vichapwe vikiwa na kauli mbiu hiyo.

Tunapenda kuutarifu umma zaidi kuwa baada ya Halmashauri kuu ya Taifa ya chama kupitisha kauli mbiu hii, ilipitishwa kuwa uzinduzi wake ufanyike Mkoani Kigoma, ambapo ilizinduliwa na Mwenyekiti wa Chama Taifa, Ndugu James Mbatia Disemba 19, 2009 tarafa ya Nguruka mkoani Kigoma.

Tumendelea kuitumia kauli mbiu hii katika ziara zote za chama tangu Disemba2009 mpaka sasa ambapo tumepita majimbo ya Kigoma kusini, Kigoma mjini, Kigoma kaskazini, Muhambwe, Kasulu magharibi, Kasulu mashariki, Buyungu na sasa Kawe ambapo wandishi wengi wa habari walishuhudia tukitumia tulipofanya mkutano wa Mwenyekiti(T) James Mbatia kutangaza nia ya Kugombea ubunge jimbo la Kawe, Machi20, 2010 pale viwanja vya Tanganyika Packers

Ni katika msingi huo tunashangazwa kuona matangazo ya CCM kuhamasisha uchagiaji wa kampeni zao wameanza kutumia kauli mbiu ya NCCR Mageuzi ya “PAMOJA, TUTASHINDA!”. Tunakitaka CCM kitumie ubunifu wake kubuni kauli mbiu yake badala ya kupora kauli mbiu ya NCCR Mageuzi. Tunawataka wasitishe mara moja kutumia kauli mbiu yetu.

Imesainiwa na;

David Kafulila
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi(T)
Simu: 0716 42 62 20.

0 comments:

Post a Comment